Sunday, May 11, 2014

TWB imetoa zaidi sh bilioni 20 kwa wanawake wajasiriamali na vijana

Benki ya Wanawake Tanzania (TWB) imetoa zaidi sh bilioni 20 kwa wanawake wajasiriamali na vijana katika jitihada za kuwawezesha kukuza mitaji na kuimarisha biashara zao nchini.
Hayo yalisemwa na Mkurugenzi Mwendeshaji wa benki hiyo, Margreth Chacha, alipozungumza na waandishi wa habari mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam kuwa katika kipindi cha chini ya miaka minne tangu benki hiyo ianzishwe, maelfu ya wajasiriamali wanawake na vijana wameshanufaika na mikopo ya kuendeleza biashara zao.


“Mikopo yetu kwa wajasiriamali hawa imekuwa kichocheo kikubwa katika kupanua wigo wa biashara zao na marejesho ya mikopo hiyo kutoka kwa wajasiriamali na vijana inaridhisha na kutia moyo,” alisema.


Chacha alisema benki yake imeona kwamba kuwawezesha wajasiriamali wanawake na vijana kuna maana kubwa katika kuchangia maendeleo na ukuaji wa shughuli za kijamii na uchumi nchini.


“Ni imani ya benki kuwa wanawake na vijana ni wachangiaji wakubwa katika uchumi wa nchi, kwani wao idadi yao ni kubwa, hivyo endapo watawezeshwa vilivyo basi wanasimama katika nafasi kubwa ya kubadilisha uchumi,” alisema.


Kwa mujibu wa mkurugenzi mwendeshaji huyo, kiasi cha sh  bilioni 17.6 zimetolewa kwa wajasiriamali na vijana kwa Mkoa wa Dar es Salaam,  sh bilioni 1.3  zimetolewa kwa wajasiriamali wa  Dodoma na  sh milioni 686  kwa wajasiriamali wa Mwanza.


“Wakati sasa tukiwa katika mpango kabambe wa kujitanua kila sehemu hapa nchini, tayari benki yetu imeshatoa mikopo ya kiasi cha shilingi milioni 178 kwa wajasiriamali na vijana mkoani Mbeya na kiasi cha shilingi milioni 366 kwa wajasiriamali vijana mkoani Ruvuma.


“Wajasiriamali katika Mkoa wa Dodoma walijiunga katika vikundi na mikopo yao waliitumia kununulia mashine za kukamulia mafuta ya alizeti ambapo wale wa mkoani Mbeya walielekeza katika manunuzi ya mashine za kulimia maarufu kwa jina la ‘power tillers’,” alisema.

Akifafanua zaidi, Chacha alisema vijana mkoani Ruvuma wamewezeshwa kupata mitaji pamoja na kuwa hawakuwa hata na kianzio, lakini benki imewawezesha.

“Vijana wapatao 80 wamewezeshwa kukopa pikipiki, bajaj na magari madogo ya kubebea mizigo, na sasa wanazifanyia biashara kubwa mkoani Ruvuma,” alisema.

0 comments:

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More

 
Design by Free WordPress Themes | Bloggerized by Lasantha - Premium Blogger Themes | Powerade Coupons