Monday, May 12, 2014

WAMILIKI WA SHULE WATAKIWA KUFANYA TATHIMINI KWENYE SHULE ZAO

Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Raymond Mushi, amewataka viongozi wa elimu pamoja na wamiliki wa shule nchini kuwa na utaratibu wa kufanya tathimini za mara kwa mara katika shule, ili kutafakari njia za kutoa elimu bora kwa wanafunzi.

Mkuu wa Wilaya ya Ilala Mushi , alitoa rai hiyo jijini Dar es Salaam jana wakati wa kutoa tuzo ya vyeti kwa shule za msingi na sekondari pamoja na wanafunzi waliofanya vizuri katika Mkoa wa Dar es Salaam katika kuadhimisha Wiki ya Elimu.


Alisema wamiliki wa shule na wadau wana dhima kubwa katika kukomboa elimu na kuhakikisha wanafikia malengo ya Matokeo Makubwa Sasa (BRN).
Alizipongeza shule zilioibuka kidedea katika mitihani ya mwaka jana ambazo ni Tusiime na St. Joseph Millenium kutoka Wilaya ya Ilala ambayo ilipata wastani wa 230, Montfort (Temeke) na Fountain of Joy (Kinondoni).


Shule nyigine ni Hazina (Kinondoni), Nyiwa, Heritage na New Ambasador (Ilala), Holy Cross (Temeke) na Anazak (Kinondoni).
“Kwa upande wa shule zetu za serikali tumejitahidi kidogo ambapo naipongeza  Zanaki, Msimbazi Mseto, Msimbazi, Boma zote kutoka Ilala, Kijitonyama Kisiwani, Mirambo na Mapambano (Kinondoni), Maktaba, Umoja wa Mataifa, Mkoani (IIala),” alisema Mushi.


Sekondari zisizo za kiserikali zilizofanya vizuri ni Thomas More Machrina, Feza Girl, Canossa, Alpha, Feza Boys, Hellen’s, St. Joseph Millennium, Rising Star na Barbro Johansson zote kutoka Wilaya ya Kinondoni pamoja na Tusiime ya  Ilala.


“Shule za serikali zilizofanya vizuri ni Jangwani, Zanaki, Benjamin William Mkapa (Ilala), Chang’ombe, Kibasila (Temeke), Pugu, Azania, Kisutu Dar es Salaam (Ilala) pamoja na Kiluvya Kinondoni,” alisema Mushi.


Alieleza changamoto zinazoikabili sekta ya elimu kuwa ni upungufu wa shule za sekondari, upungufu wa walimu masomo ya Hisabati na Sayansi, uchakavu wa miundombinu pamoja na ufaulu wa chini wa wanafunzi wanaohitimu mafunzo katika ngazi mbalimbali.


“Kuna upungufu wa vyumba vya madarasa 4,314 kwa sekondari, matundu ya vyoo 16,046, na madawati 76,029. Kwa upande wa shule za msingi kuna upungufu wa madarasa 1,020, matundu ya vyoo 3,531 na madawati 35,420 kwa shule za serikali za sekondari,” alisema.

0 comments:

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More

 
Design by Free WordPress Themes | Bloggerized by Lasantha - Premium Blogger Themes | Powerade Coupons