Saturday, May 17, 2014

WATU 10 WAFARIKI DUNIA 70 WAJERUHIWA.


Kutokea kwa bomu lililo lipuka jana inalipotiwa kuwa  Watu 10 wamefariki dunia na wengine zaidi ya 70 kujeruhiwa baada milipuko miwili kutokea karibu na soko kubwa la nguo la Gikomba mjini Nairobi nchini kenya.
Kuna uwezekano idadi hiyo ya watu waliofariki dunia ikaongezeka kutokana na hali ya baadhi ya majeruhi kuwa mbaya zaidi.
Milipuko hiyo imetokea siku moja baada ya nchi za magharibi ikiwamo Uingereza kuwataka raia wake wanaoishi nchini humo kurejea nyumbani kwa hofu ya usalama.
Jeshi la polisi limesema kuwa linamshikilia mtu mmoja kwa madai ya kuhusika kwenye tukio hilo na hakuna taarifa zaidi zilizotolewa.


Msemaji wa Hospitali ya Kenyatta aliliambia Shirika la Habari la AFP kuwa baadhi ya majeruhi waliopelekwa hospitalini hapo hali zao ni mbaya.
Mfanyabiashara mmoja aliyekuwepo kwenye eneo la tukio alisema kuwa alisikia mlio mkubwa uliofuatiwa na moshi uliotanda eneo lote la soko na kwamba baada ya tukio hilo watu wengi walikimbia ovyo kuokoa maisha yao.


“Watu wengi wamejeruhiwa. Sijui idadi ya watu waliopoteza maisha, lakini kusema kweli mlipuko huu ni mkubwa na utakuwa umeleta madhara makubwa,” alisema Mwangi Maina.


Hadi sasa hakuna kundi lililodai kuhusika na tukio hilo, lakini wachunguzi wa mambo wanalitaja Kundi la Al-Shabaab kuwa huenda likawa nyuma ya matukio hayo.
Kenya imekuwa ikiandamwa na matukio ya kigaidi tangu ilipopeleka askari wake nchini Somalia kukabiliana na kundi lenye msimamo mkali wa Kiislamu, Al-Shabaab.
Taarifa zilizotolewa na vyombo vya habari vya nchi za magharibi zinasema kuwa zaidi ya watu 100 wamepoteza maisha katika kipindi cha miezi 18 iliyopita tangu Kenya ianze kuandamwa na mashambulizi ya kigaidi.


Milipuko hiyo imekuja huku raia wengi wa kigeni waliokuwa nchini Kenya kwa shughuli za utalii wakiwa wanarejea nyumbani kuitika wito uliotolewa na serikali zao.
Tahadhari hiyo kutoka kwa Serikali ya Uingereza ilieleza kuwa askari wa Al-Shabaab, huenda wakafanya mashambulizi nchini Kenya katika muda wowote kuanzia sasa.
Taarifa hiyo iliwaonya raia wote wa Uingereza ambao wako nchini Kenya kwa shughuli ambazo siyo za dharura waondoke nchini humo.


Marekani, Ufaransa na Australia pia zimewataka raia wao walioko eneo la Pwani ya Kenya kuondoka mara moja.
Al-Shabaab imeimarisha mashambulizi katika eneo hilo katika siku za hivi karibuni huku likisisitiza kuwa linafanya hivyo kama njia ya kulipiza kisasi kutokana na Kenya kupeleka majeshi yake nchini Somalia.

0 comments:

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More

 
Design by Free WordPress Themes | Bloggerized by Lasantha - Premium Blogger Themes | Powerade Coupons